The Chant of Savant

Wednesday 18 April 2012

Siku nikifa, nataka prezidaa asile chakula


Alikuwa na nyumba ndogo
Mungu muweke pema peponi
Alikuwa akibwia unga
Mungu muweke pema peponi
Alikuwa kiwembe
Mungu muweke pema peponi
Alikuwa fisadi
Mungu weka pema peponi
Alikuwa tapeli
Mungu ficha pema peponi
Wewe ni mwenye huruma

Huu wimbo hata kama una ‘tune’ nzuri bado unanisuta, acha niachane nao nianze kuwaza mipango yangu ya kuukwaa na kuwa mtu maarufu sana Kayani. Ngoja nisukuti kwanza.
Baada ya kushuhudia msiba wa Stivu Kanumbu hivi karibuni na jinsi wazito walivyojifanya wanamzimia wakati walikuwa wakificha aibu ya Arushameru, Mpayukaji napanga kuwa mcheza sinema za Kiswahili.
Msiniulize mambo ya maadili ya Kibongo. Mie nitacheza sinema hasa zile za ‘X’ ili nipendwe.
Nitachukua vidosho kama sina akili. Maana ukiwa supastaa tena kijogoo utaheshimika sana kuwa wewe ni dume la mbegu, ambalo likiamua kusia mbegu unaweza kuzalisha wanaharamu wengi wenye vipaji kama vyako.
Isitoshe kwa vile kaya yetu inapenda sana mambo ya ngono, usipopenda ngono unaonekana kama mtoto si riziki. Ukiwa supastaa unakuwa na haki ya kuchafua kila ua. Unaruka toka hili kwenda lile.
Nataka nikidedi prezidaa, nkewe, waziri mkubwa, Makamo wa prezidaa na wakubwa wengine waniombolezee na kutangaza siku kumi za maombolezo kitaifa huku bendera zikipepea robo mlingoti kutokana na utukufu wangu. Katika Kaya ya majuha kila kitu kinawezekana. Hamjaona wawekezaji waliotoka kwa Mobutu kuja kuwekeza kwenye kuharibu mila zenu mnavyowaabudu na kuwapa ulaji wakati walipaswa kuwa lupango?
Natamani nidedi wakati wa vikao vya waheshimiwa kule Idodomya ili kamera za runinga ziwashiti na kuja kurekodi msiba wangu. Unadhani ukiwa mcheza sinema saizi yangu ni mchezo? Unakuwa mkubwa kuliko hata wadharauliwa na vikao vyao vya ulaji. unazikwa kwa mbwembwe na makandokando yake kuliko hata mkuu wa masoja.
Nani alikuwa na hamu ya kumtangaza Jenero Kyaro alipodedi zaidi ya Lulu? Kwani hamkuona au hamna kumbukumbu? hamkuona mibaba mizima iliyokimbia wajibu wa kuwale watoto ilivyokuwa ikijishebedua kudai ni mizazi ya hao masupastaa uchwara wenu?
Hamkuona kwenye msiba wa Kanumbu? Hapakuwa na cha mheshimiwa microphone au mheshimiwa twitter wala nini zaidi ya vimwekumweku vyote kuelekezwa makaburini. Magazeti yote yatageuka ya udaku na yataandika habari na utukufu wangu.
Yale ya udaku yatapata mabilioni ya madafu kwa miaka mitatu kwa kuendelea kuuza uongo juu ya maisha yangu. Acha Yesu ajisemee kuwa waache wafu wazike wafu wenzao. Maana kama mtu huna busara una hasara na hasara yenyewe kubwa kuliko hata kifo. Anyway, usanii ndiyo huu. Lazima wasanii wakumbukane hata kama wote hawaigizi sinema za aina moja. Hata hivyo sinema ni sinema iwe ya siasa au ya matusi bado ni sinema. na wote ni wasanii yaani wanaofanya vitu vya kubuni kuwapumbaza majuha.
Nataka prezidaa siku nikidedi asile chakula wala kulala achia mbali kuahirisha miruko yake. siku nikifa, prezidaa lazima aamuru majeshi kunipigia mizinga mia na kuhakikisha nazikwa kwenye viwanja vya ikuu.
Hamkusikia wapuuzi wakisema eti yatafutwe makaburi ya watu mashuhuri na watu hao wasiishi uswazi wakati walizaliwa huko huko. Eti nao hao ni wabunge? Kaya inapelekwa wapi hii iwapo mjengoni wanajazana wahuni na mafisadi watupu?
Wale wachache wenye akili naona wanapigwa mapanga na mapilato wa kisiasa kina Rwaki, Voda Fasta na awamu ya four. Mara hii mmesahau kesi ya Godibless Rema na Dk. Bat-leader Biriani ambaye alishinda kesi hata bila kuifungua wala kukanyaga kwa pilato.
Mapilato wetu nao siku hizi wamekuwa kama vyangu. Hayo tuyaache. Anyway siwatukani bali naongea kama Amicus Curriae yaani rafiki wa haki kwa wale waliosoma sheria.
Nimeongea na Eddi Mafi amesema atanipiga tafu kwa kuhamia Bongolaland tukidedi tupewe maujiko hata tusiyostahili.
Maana kule kwa Joji Kichaka alipokufa Jako Wako bwana Braaack Obamiza hata hakujali zaidi ya kutoa salamu kiduchu. Angeendaje wakati yeye siyo waziri wa sanaa na sinema? Wenzetu wanaheshimu protokali sana. Nasikia siku alipodedi Kanumbu, Pedeejee hakwenda popote, badala yake alijikita kwenye msiba ili aonekane anawapenda wabaya wake anaowauza kwa wachukuaji kila uchao. Ajabu walevi hawakumshtukia zaidi ya kumsifia eti ni kipenzi cha watu. Angewapenda si angewaedeleza.
Kwa sababu siasa zimegeuka umachinga, nikidedi vyama vya siasa vitatuma salamu za rambirambi ili kuwaaminisha wapiga kura kuwa vinapenda watu kama hawa wabaya wao watakaotumia msiba wangu kutangaza sanaa zao.
Hata madhehebu ya dini kwa vile nayo yanafanya siasa, yatatuma viongozi kuja kuniombea hata kama kifo changu kitatokana na uzinzi au ubakaji. Ukishakuwa supastaa huwezi kutenda kosa lolote mbele ya wajinga wanaokuabudia. Hivyo usupastaa hasa wa Kiswahili ni kibali tosha cha kufanya madudu na watu wakayashabikia.
Natamani nidedi wakati bei ya wese imepanda. Najua hakuna atakayeandika habari za kupanda wese wala gharama za maisha zaidi ya kifo changu. why should they care if they just live like flukes?
Siku nyingine nitawaambia. Hamkuwasikia baadhi ya wenye akili mgando wakidai kuwa jamaa aliyededi hadi kunifanya niwazie usanii eti alipaswa kuwa na bodigadi na hakupaswa kuishi uswazi wakati alizaliwa na kukulia uswekeni achia mbali uswazi?
Hawa hawapaswi kupewa heshima yoyote zaidi ya kuwa malimbukeni na wapuuzi wa kawaida. Masa Mulalata upo hapo na pendekezo lako la kihiyo? Mie nikiwa supastaa nitaishi uswazi kwa vile nilizaliwa uswazi. Tutaonana nikirudisha namba.
Chanzo: Tanzania Daima April 18, 2012.

No comments: